Trump amteua Seneta JD Vance kuwa mgombea mwenza

  • | VOA Swahili
    380 views
    Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump amesema Seneta wa Ohio James David Vance (JD) Vance, mwenye umri wa miaka 39, ndiye chaguo lake la mgombea mwenza kuelekea uchaguzi wa mwezi Novemba. Trump alisema kupitia ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa Truth Social: “Baada ya kutafakari na kufikiria kwa muda mrefu, na kwa kuzingatia vipaji vya hali ya juu vya wengine wengi, nimeamua kwamba mtu anayefaa zaidi kushika wadhifa huop ni JD Vance wa jimbo la Ohio." Kongamano la Kitaifa la Chama cha Republican lilianza wiki hii, huku wajumbe na maafisa wakiwasili mjini Milwaukee, Wisconsin wakati kukiwa na msukosuko uliofuatia jaribio la kumuua Trump Jumamosi. Trump anatarajiwa kuteuliwa rasmi kuwa mgombea urais kwa tikiti ya chama cha Republikan. Shirika la habari la AFP linaripoti kuwa kupanda kwa J.D. Vance hadi mgombea mwenza wa Donald Trump kunakamilisha mabadiliko makubwa kwa seneta huyo, ambaye sasa anaonekana kuwa sura ya baadaye ya chama cha Republican. Vance amekuwa mmoja wa watatezi wakubwa wa Trump katika bunge, akiunga mkono sera mbalimbali zenye utata kama vile kupinga uhamiaji, kusisitiza Ukristo kama njia ya kukuza maadili ya umma na ya kibinafsi, na kupinga vita vya Ukraine dhidi ya uvamizi wa Russia. Mapema mwaka huu, seneta huyo wa Ohio alionya wale ambao hawamuungi mkono Trump kwamba "ana kumbukumbu ya muda mrefu." "Kama unampinga Trump na wale anaowaunga mkono, usitegemee msaada wangu," alisema. Hata hivyo, Vance katika siku za nyuma alikuwa mkosoaji wa Trump, na wakati mmoja alimuita "Hitler wa Marekani," kwa mujibu wa shirika la habari la AFP. #donaldtrump #marekani #republikan #chama #jdvance #jimbo #ohio #milwaukee #wisconsin #raiswazamani